Hamia kwenye habari

NOVEMBA 17, 2020
MSUMBIJI

Kitabu cha Mathayo Chatolewa Katika Lugha ya Kitonga na Kironga

Kitabu cha Mathayo Chatolewa Katika Lugha ya Kitonga na Kironga

Novemba 14 na 15, 2020, Biblia—Injili ya Mathayo ilitolewa katika mfumo wa kielektroni katika lugha ya Kitonga na Kironga, lugha mbili zinazozungumzwa kusini mwa Msumbiji. Kutolewa kwa kitabu hicho cha Biblia ni zawadi kutoka kwa Yehova iliyofika kwa wakati kwa wahubiri 524 wanaozungumza Kitonga na wahubiri 1,911 wanaozungumza Kironga.

Ndugu Amaro Teixeira, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Msumbiji, alitoa tafsiri hizo kupitia programu iliyorekodiwa mapema na kutazamwa baadaye na wahubiri. Kwa kuongezea, ndugu zetu walipewa ruhusa ya kuonyesha programu hiyo kupitia televisheni ya nchi hiyo na vituo mbalimbali vya redio katika eneo hilo. Kwa kuwa wasomaji wengi hawana vifaa vya kielektroni, kitabu hicho cha Mathayo chenye kurasa 64 kitachapishwa pia.

Ndugu Teixeira anasema hivi: “Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia hayapatikani kwa urahisi katika lugha hizi. Tuna furaha sana kwamba sasa tuna kitabu cha Mathayo, kwa kuwa injili hiyo ina masimulizi ya ukoo wa Yesu na kuzaliwa kwake, Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, na unabii wake wa pekee aliotoa kuhusu siku za mwisho.”

Akizungumzia manufaa ya tafsiri hii iliyo sahihi na inayoeleweka kwa urahisi, mtafsiri mmoja alisema hivi: “Kuna mafundisho mengi katika kitabu cha Mathayo. Nina uhakika kwamba wasomaji wengi watatoka machozi ya shangwe watakapokuwa wakisoma Mahubiri ya Mlimani katika lugha yao ya mama.”

Wataalamu wanasema kwamba watu 224,000 hivi wanazungumza Kitonga na wengine 423,000 hivi wanazungumza Kironga. Tunatumaini kwamba tafsiri hizi za Biblia zitawasaidia watu wengi zaidi kuipata “barabara inayoongoza kwenye uzima.”—Mathayo 7:14.