Hamia kwenye habari

JUNI 18, 2020
INDIA

Watafsiri Nchini India Wanaendelea na Kazi Licha ya Changamoto

Watafsiri Nchini India Wanaendelea na Kazi Licha ya Changamoto

Ugonjwa wa corona umetokeza changamoto za pekee kwa Ofisi za Utafsiri (RTO) 11 nchini India, zinazotafsiri machapisho yetu katika lugha 36. Kwa msaada wa Yehova, vikundi vya utafsiri vinaendelea kukabiliana na changamoto hizo wanapoendelea na kazi.

Kazi ya utafsiri inategemea sana ushirikiano. Hata hivyo, kwa kuwa ugonjwa wa corona unazidi kuenea, India iliweka sheria iliyowakataza wananchi wake kutotoka nyumbani kabisa, jambo linalofanya iwe vigumu kwa watafsiri kukutana ili kufanya kazi pamoja. Pia, wale waliokuwa wakirekodi sauti na video hawangeweza kufanya kazi yao ndani ya ofisi za utafsiri.

Katika ofisi za utafsiri, watu walianza kutumia video kuwasiliana na kurekodi video na sauti badala ya kukutana na kufanya kazi pamoja. Njia hizi mbadala zimewasaidia sana watafsiri kusaidiwa kazi na ndugu na dada wa nchi nyingine kama vile Bangladesh na Marekani.

Ndugu hao wamebuni pia njia za kutayarisha video za lugha ya ishara huku wakihakikisha kwamba hawakaribiani wanapofanya kazi. Baadhi ya watafsiri wametumia vyumba vyao vya kulala kama studio na wanatumia vifaa walivyo navyo kufanyia kazi. Wanatumia maboksi ili kuwekea kamera na kamera ya simu badala ya kamera za hali ya juu.

Kwa kuongezea, watafsiri hao wanamtegemea Yehova ili awasaidie waendelee kuwa imara na wenye bidii katika kipindi hiki. Baadhi yao walisema hivi:

Ndugu Jose Francis anayeishi Kolkata alisema: “Tunapokabili hali ngumu, wanadamu wanaweza kuona ukuta, lakini Yehova anaona njia ya kuzunguka ukuta huo.”

Dada Bindu Rani Chandan anayeishi Bangalore alisema: “Kujua kwamba Yehova ananitumia katika pindi hii ngumu kunanipa shangwe kubwa licha ya changamoto tunazokabili.”

Dada Rubina Patel anayeishi Vadodara alieleza hisia zake hivi: “Hakuna kinachoweza kumzuia Yehova na tengenezo lake—hata virusi vya corona haviwezi.”

Tunajivunia kuwa na ndugu na dada wanaofanya kazi ya utafsiri kwa bidii. Tuna uhakika kwamba roho takatifu ya Yehova yenye nguvu imewasaidia wapate mafanikio na kwamba kwa roho yake hiyo, unabii huu wa Yesu hakika utatimia: “Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.”—Mathayo 24:14.