Hamia kwenye habari

JULAI 21, 2014
AUSTRIA

Mashahidi wa Yehova Waheshimiwa Kwenye Makumbusho ya Kambi ya Mateso ya Gusen

Mashahidi wa Yehova Waheshimiwa Kwenye Makumbusho ya Kambi ya Mateso ya Gusen

SELTERS, Ujerumani—Jumapili, Aprili 13, 2014, Makumbusho ya Kambi ya Mateso ya Gusen nchini Austria iliweka jiwe la makumbusho kama ishara ya kuwatambua Mashahidi wa Yehova wapatao 450 waliofungwa na Wanazi kwenye kambi ya mateso ya Mauthausen na kwenye kambi yake ndogo ya Gusen. Wageni zaidi ya 130 walihudhuria tukio hilo.

Jiwe la makumbusho lililowekwa wakati wa sherehe ya umma iliyofanywa kwenye Makumbusho ya Kambi ya Mateso ya Gusen, Aprili 13, 2014.

Mashahidi walipowasili kwenye kambi ya mateso ya Mauthausen, kamanda mkuu aliwatisha hivi: “Hakuna Mwanafunzi wa Biblia atakayeondoka hapa akiwa hai.” Martin Poetzinger, aliyeokoka kifungo cha miaka tisa gerezani huko Dachau, Mauthausen, na Gusen kisha baadaye akatumika akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, alisema hivi kuhusu maisha yake katika kambi ya Mauthausen: “Gestapo walijaribu kila njia ili wavunje imani yetu.”

Mei 1945: Kambi ya Mateso ya Gusen. Martin Poetzinger (aliyeketi mbele, wa pili kutoka kushoto) pamoja na waokokaji wenzake 23 muda mfupi baada ya kuachiliwa huru.

Baadaye, baadhi ya Mashahidi hao walihamishwa hadi kwenye kambi ndogo ya Gusen. Gusen ilitumiwa hasa kama “kambi ya mauaji,” ambamo kila siku, kulipangwa njama za kuua watu kimakusudi. Ili waendelee kuwa na imani yenye nguvu, Mashahidi walikutana usiku katika vikundi vidogo ili kuzungumzia mistari ya Biblia waliyokumbuka. Pindi moja, walipata Biblia. Waliigawanya vipande-vipande, na kila Shahidi alisoma na kubadilishana na mwenzake kurasa hizo. Walificha vipande hivyo chini ya vitanda vyao na kutumia kila fursa waliyopata ili kuvisoma.

Kwa busara, Mashahidi hao waliwaambia pia wengine ujumbe wa Biblia. Wafungwa watano kutoka Poland walijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na kubatizwa kisiri katika chombo cha mbao kilichotengenezwa hususa kwa kusudi hilo. Shahidi aitwaye Franz Desch alimhubiria ofisa mmoja wa SS ambaye baadaye alikuja kuwa Shahidi wa Yehova.

Wolfram Slupina, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Austria, anasema hivi: “Tunathamini sana kwamba Mashahidi wanakumbukwa kwa sababu ya imani na ujasiri wao walipokuwa katika kambi ya Mauthausen na ya Gusen. Azimio lao la kumtendea kila mtu kwa huruma na fadhili za Kikristo lilikuwa ushindi mkubwa dhidi ya uovu, na hilo linastahili kukumbukwa na kuigwa.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000

Austria: Wolfram Slupina, simu +49 6483 41 3110