Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

TUIGE IMANI YAO ENOKO

‘Alimupendeza Mungu Vema’

‘Alimupendeza Mungu Vema’

ENOKO aliishi miaka mingi. Inaweza kuwa nguvu kwetu kuamini, lakini mwanaume huyo aliishi miaka 365 hivi; hiyo ni zaidi ya mara 4 tukilinganisha na urefu wa miaka yenye mutu anaweza kuishi leo! Lakini hakuwa kabisa mukubwa tukimulinganisha na watu wa wakati wake. Miaka zaidi ya 5000 yenye imepita, watu waliishi miaka mingi sana kuliko leo. Adamu, mwanaume wa kwanza, alikuwa na miaka zaidi ya 600 wakati Enoko alizaliwa, na Adamu aliishi tena miaka 300 ingine! Wazao fulani wa Adamu waliishi miaka mingi zaidi kuliko yeye. Kwa hiyo, Enoko mwenye alikuwa na miaka 365, angeonekana kuwa angali na nguvu kabisa na siku nyingi za kuishi. Lakini, haikuwa hivyo.

Inaonekana Enoko alikuwa katika hatari ya kifo. Umuwazie katika akili yako namna anakimbia, ametoka tu kuambia watu ujumbe wa Mungu, na anaendelea kuwaza namna watu hao walitenda kisha kusikia ujumbe huo. Sura za watu hao zilionyesha kama wanakasirika sana. Watu hao walimuchukia. Walizarau ujumbe wake, na walichukia sana Mungu mwenye alimutuma. Hawangeweza kumushambulia Yehova, Mungu wa Enoko, lakini wangeweza kumushambulia mwanaume huyo! Pengine Enoko alijiuliza ikiwa angeona tena familia yake. Alikumbuka bibi yake na watoto wake wanawake ao mutoto wake Methusela ao Lameki mutoto wa Methusela? (Mwanzo 5:21-23, 25) Huo ulikuwa mwisho wake?

Biblia haizungumuzie sana Enoko. Ni maandiko matatu mafupi ndiyo tu yanamuzungumuzia kwa kifupi. (Mwanzo 5:21-24; Waebrania 11:5; Yuda 14, 15) Hata hivyo, maandiko hayo yanatoa maelezo ya kutosha ili kutusaidia kuona kama alikuwa mwanaume mwenye imani kubwa. Unahangaikia mahitaji ya kimwili ya familia yako? Umekwisha kupata magumu kwa sababu ya kupenda kushikamana na mambo yenye unaona kuwa sawa? Kama jibu lako ni ndiyo, imani ya Enoko inaweza kukusaidia sana.

‘ENOKO ALIENDELEA KUTEMBEA PAMOJA NA MUNGU WA KWELI’

Watu walikuwa na matendo ya mubaya wakati Enoko alizaliwa. Hicho kilikuwa kizazi cha saba cha Adamu. Kwa kweli, watu wa wakati huo walikuwa karibu na ukamilifu wenye Adamu na Eva walikuwa nao na kisha wakaupoteza. Ndiyo sababu watu waliishi miaka mingi sana wakati huo. Lakini, walikuwa na hali ya mubaya sana ya kiroho na walikuwa na matendo ya mubaya sana. Jeuri ilikuwa imeenea. Hali hiyo ilianza katika kizazi cha pili, wakati Kaini alimuua ndugu yake Abeli. Inaonekana kwamba mutu fulani wa kizazi cha Kaini alijisifu kuwa mwenye jeuri zaidi na mwenye kulipiza kisasi zaidi kuliko Kaini! Katika kizazi cha ine, ubaya mwingine ulitokea. Watu walianza kuliitia jina la Yehova, lakini haiko ili kumutolea ibada kwa heshima. Walikuwa wanatumia jina takatifu la Mungu katika njia ya mubaya, yenye kukosa heshima.​—Mwanzo 4:8, 23-26.

Dini hiyo ya uongo ilienea sana wakati wa Enoko. Wakati Enoko alikuwa anakomaa alipaswa kuchagua. Angefuata watu hao wa wakati wake? Ao angetafuta Yehova, Mungu wa kweli mwenye aliumba mbingu na dunia? Habari ya Abeli, mwenye alikufia imani yake kwa sababu ya kumuabudu Yehova katika njia ya muzuri, ilipaswa kumuchochea sana. Enoko alichagua kufuata mufano wa Abeli. Mwanzo 5:22 inatuambia hivi: ‘Enoko aliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli.’ Maneno hayo ya ajabu yanaonyesha kwamba Enoko alikuwa mutu mwenye imani ambaye aliishi katika dunia ya watu wenye hawakuwa wanamuogopa Mungu. Yeye ni mutu wa kwanza mwenye Biblia inazungumuzia hivyo.

Andiko hilohilo linasema kwamba Enoko aliendelea kutembea pamoja na Yehova kisha Methusela, mutoto wake kuzaliwa. Kwa hiyo, Enoko alikuwa baba wa familia wakati alikuwa na miaka 65 hivi. Alikuwa na bibi, mwenye Biblia haitaje jina lake, na hesabu yenye haijulikane ya “wana na mabinti.” Ikiwa baba anatembea pamoja na Mungu wakati anakomalisha watoto wake na kutimiza mahitaji ya familia yake, anapaswa kufanya hivyo katika njia yenye kumupendeza Mungu. Enoko alielewa kama Yehova alipenda abakie muaminifu kwa bibi yake. (Mwanzo 2:24) Na alifanya yake yote ili kufundisha watoto wake kumuhusu Yehova Mungu. Matokeo ilikuwa nini?

Biblia hailete mafasirio ya mingi juu ya jambo hilo. Haiseme kitu juu ya imani ya Methusela, mutoto wa Enoko, mwenye aliishi miaka mingi sana kati ya watu wenye kutajwa katika Biblia; alikufa mwaka wenye Garika kubwa ilitokea. Hata hivyo, Methusela alifikia kuwa baba ya mutoto mwenye kuitwa Lameki. Lameki aliishi zaidi ya miaka 100 pamoja na Enoko, tate yake. Na Lameki aliendelea kuonyesha imani kubwa. Yehova alimuongoza ili kutoa unabii fulani kuhusu Noa, mutoto wake, na unabii huo ulitimia kisha Garika. Kama Enoko, baba ya tate yake, Noa alikuwa tofauti na watu wengine kwa sababu alitembea pamoja na Mungu. Noa hakumuonaka Enoko hata siku moja. Lakini Enoko aliacha uriti muzuri sana. Pengine Noa alijifunza kuhusu uriti huo kupitia baba yake Lameki, ao kupitia tate yake Methusela ao pengine kupitia Yaredi, baba ya Enoko, mwenye alikufa wakati Noa alikuwa na miaka 366.—Mwanzo 5:25-29; 6:9; 9:1.

Fikiria kidogo tofauti kati ya Enoko na Adamu. Hata kama alikuwa mukamilifu, Adamu alimukosea Yehova na akaachia wazao wake uriti mubaya, ni kusema, uasi na mateso. Lakini hata kama hakuwa mukamilifu, Enoko alitembea pamoja na Mungu na akaachia wazao wake uriti muzuri, ni kusema, imani. Adamu alikufa wakati Enoko alikuwa na miaka 308. Wazao wa Adamu walifanya kilio kwa ajili yake, baba huyo mwenye kujipenda mwenyewe? Hatujue. Hata hivyo, Enoko ‘aliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli.’—Mwanzo 5:24.

Kama unahangaikia mahitaji ya familia yako, ona mambo yenye imani ya Enoko inaweza kukufundisha. Hata kama ni jambo la lazima kuhangaikia mahitaji ya kimwili ya familia yako, ni jambo la maana hata zaidi kuhangaikia mahitaji ya kiroho ya familia yako. (1 Timotheo 5:8) Unaweza kufanya hivyo kupitia maneno na matendo yako. Kama unaamua kutembea pamoja na Mungu kama Enoko kwa kuacha kanuni za Mungu ziongoze maisha yako, wewe pia unaweza kuachia watu wa familia yako uriti muzuri, ni kusema, mufano muzuri wenye wanaweza kufuata.

ENOKO “ALITOA UNABII KUWAHUSU”

Pengine Enoko alijiona kuwa peke yake katika ulimwengu wa watu wenye kukosa imani. Lakini, Yehova, Mungu wake alitambua kama alikuwa na imani? Ndiyo. Siku moja Yehova alizungumuza na mutumishi wake huyo muaminifu. Mungu alimupatia ujumbe wenye alipaswa kutangazia watu wa wakati wake. Kwa hiyo, Mungu alimufanya Enoko kuwa nabii; ujumbe wake ndio wa kwanza kuzungumuziwa katika Biblia. Tunajua jambo hilo kupitia Yuda, ndugu ya Yesu, mwenye aliongozwa na roho ya Mungu ili kuandika maneno ya unabi wa Enoko miaka mingi sana kisha hapo. *

Enoko alitoa unabii gani? Unabii huo unasema hivi: ‘Tazama! Yehova alikuja pamoja na watakatifu wake makumi ya maelfu, ili kufanya hukumu juu ya wote, na kuwasibitisha kuwa ni wenye hatia wote wasiomuogopa Mungu kuhusu matendo yao yote ya kutomuogopa Mungu ambayo walitenda kwa njia ya kutomuogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kushtua ambayo watenda-zambi wasiomuogopa Mungu walisema juu yake.’ (Yuda 14, 15) Jambo la kwanza unaweza kuona ni hili: Enoko alitumia maneno yenye kuonyesha wakati uliopita, ni kama vile Mungu alikuwa amekwisha kutimiza unabii huo. Unabii mwingi wenye ulifuata uliandikwa hivyo. Wazo kubwa ni hili: Nabii anazungumuzia jambo lenye iko hakika kwamba litatokea, kwa hiyo, jambo hilo linaweza kuzungumuziwa kwa njia yenye kuonyesha kama limekwisha kutokea!—Isaya 46:10.

Bila woga, Enoko alitangazia ulimwengu wenye jeuri ujumbe wa Mungu

Namna gani Enoko alitangaza ujumbe huo? Pengine kwa kuhubiria watu wote wenye walikuwa na uwezo wa kusikia? Ona namna angalisho lenye alitoa lilikuwa nzito: mara ine anatumia neno ‘kutomuogopa Mungu’ ili kuonyesha matendo yao. Kwa hiyo, unabii huo ulionya watu wote kwamba ulimwengu wenye walikuwa wamejifanyia tangu Adamu na Eva kufukuzwa katika shamba la Edeni ulikuwa umeharibika sana. Ulimwengu huo ungepata mwisho mubaya sana wakati Yehova angekuja na “watakatifu wake makumi ya maelfu,” ni kusema, maelfu ya malaika wenye nguvu sana ili kuleta uharibifu. Bila kuogopa, Enoko alitangaza ujumbe huo wa Mungu, na alifanya kazi hiyo yeye mwenyewe! Pengine kijana Lameki alishangaa kuona ujasiri wa tate yake. Kama ni hivyo, tunaweza kuelewa sababu yenye ilimufanya ashangae.

Imani ya Enoko inaweza kutuchochea kujiuliza ikiwa mawazo yetu juu ya ulimwengu huu yanapatana na mawazo ya Mungu. Hukumu yenye Enoko alitangaza bila woga wakati wake inahusu pia ulimwengu wa leo. Kama vile unabii wa Enoko ulisema, Yehova alileta Garika kubwa juu ya ulimwengu wa wakati wa Noa wenye ulikuwa na watu wenye hawamuogope Mungu. Hilo linaonyesha uharibifu mukubwa zaidi wenye utatokea karibuni. (Mathayo 24:38, 39; 2 Petro 2:4-6) Kama wakati huo, leo Mungu pamoja na malaika wake wengi wako tayari kuleta hukumu ya haki juu ya ulimwengu huu wenye haumuogope Mungu. Kila mumoja wetu anapaswa kukamata kwa uzito angalisho lenye Enoko alitoa na kulitangazia wengine. Watu wa familia yetu na marafiki wanaweza kuwa na musimamo wenye kuwa tofauti na wetu. Wakati fulani tunaweza kuona kama tuko peke yetu. Lakini Yehova hakumuacha Enoko; hataacha pia watumishi wake waaminifu leo!

“ALIHAMISHWA ILI ASIONE KIFO”

Maisha ya Enoko yaliisha namna gani? Kifo chake ni chenye kushangaza zaidi kuliko hata maisha yake. Habari ya kitabu cha Mwanzo inasema tu hivi: ‘Enoko aliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli. Kisha hakuwapo tena, kwa maana Mungu alimuchukua.’ (Mwanzo 5:24) Mungu alimuchukua Enoko namna gani? Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Kwa imani Enoko alihamishwa ili asione kifo, naye hakupatikana popote kwa sababu Mungu alikuwa amemuhamisha; kwa maana kabla ya kuhamishwa kwake alikuwa ametolewa ushahidi kwamba alimupendeza Mungu vema.’ (Waebrania 11:5) Paulo alipenda kusema nini wakati aliandika maneno “alihamishwa ili asione kifo”? Tafsiri fulani za Biblia zinasema kama Mungu alimupeleka Enoko mbinguni. Lakini hilo haliwezekane. Biblia inaonyesha kwamba Yesu Kristo ndiye alikuwa wa kwanza kufufuliwa ili kuishi mbinguni.—Yohana 3:13.

Kwa hiyo, ni katika maana gani Enoko “alihamishwa ili asione kifo”? Inaonekana kwamba, kwa upendo, Yehova alihamisha uzima wa Enoko katika kifo ili maadui wake wasimuue bila huruma. Lakini kwanza Enoko alitolewa ‘ushahidi kwamba alimupendeza Mungu vema.’ Namna gani? Mbele tu ya kifo chake, pengine Enoko alipewa maono kutoka kwa Mungu, yenye yalionyesha dunia yenye kuwa paradiso. Kupitia alama hiyo yenye kuonyesha kwamba Yehova anamukubali, Enoko akalala usingizi katika kifo. Kuhusu Enoko na wanaume na wanawake wengine waaminifu, mutume Paulo aliandika hivi: “Katika imani hawa wote walikufa.” (Waebrania 11:13) Inawezekana kisha hapo maadui wake walitafuta mwili wake, lakini ‘haukupatikana popote,’ pengine Yehova alifanya upotee ili wasiutendee mubaya ao kuutumia katika ibada ya uongo. *

Tukiwa na mawazo hayo ya Biblia katika akili yetu, sasa tujaribu kufikiria namna pengine maisha ya Enoko yaliisha. Waza kidogo katika akili yako mufano huu, lakini kumbuka kama pengine mambo haikuwa vile. Enoko iko anakimbia, na anachoka sana. Maadui wake wanamukimbiza, na ni wenye kukasirika sana kwa sababu ya ujumbe wake wa hukumu. Enoko anapata nafasi fulani ya kujificha na kupumuzika kidogo, lakini anajua kama hawezi kuponyoka tena. Maadui wake wako karibu kumuua bila huruma. Anasali kwa Mungu wake wakati anapumuzika. Kisha anasikia amani kubwa inamushukia. Anapelekwa mbali katika maono yenye kufurahisha, ni kama vile alikuwa huko kabisa.

Pengine Enoko alikuwa anapambana na hatari ya kifo wakati Yehova alimuchukua

Wazia kama vile mulango unafunguliwa mbele yake na anaona dunia yenye kuwa tofauti sana na dunia yenye alijua. Inaonekana kuwa yenye kupendeza kama shamba la Edeni, lakini hakuna makerubi wenye kuichunga ili watu wasiingie ndani. Wanaume na wanawake wengi wako na afya ya muzuri sana na wako na nguvu ya ujana. Wote wanaishi kwa amani. Hakuna hata alama ya chuki na mateso ya dini kama vile alijua zamani. Enoko anaona kama Yehova anamuhakikishia kwamba anamupenda na kumukubali. Anajisikia katika usalama, na anaona kwamba hiyo itakuwa makao yake. Wakati anajisikia kuwa na amani zaidi na zaidi, Enoko anafunga macho yake na analala usingizi kabisa, usingizi wenye hauna ndoto.

Na mupaka leo iko katika usingizi huo, na iko katika kumbukumbu la Yehova Mungu! Kama vile Yesu aliahidi, kutakuwa siku watu wote wenye kuwa katika kumbukumbu la Mungu watasikia sauti ya Kristo na kutoka katika makaburi, na kuona dunia mupya yenye kupendeza na yenye amani.​—Yohana 5:28, 29.

Utapenda kuwa katika dunia hiyo? Wazia namna utafurahi kumuona Enoko. Fikiria mambo mengi ya ajabu yenye tutajifunza kutoka kwake! Atatuambia ikiwa mambo yenye tumewazia juu ya mwisho wa maisha yake yanafanana kidogo na mambo yenye yalitokea kabisa. Lakini kuko jambo la maana sana lenye tunajifunza kutoka kwake tangu sasa. Kisha kuzungumuzia Enoko, Paulo aliendelea kusema hivi: ‘Bila imani haiwezekane kamwe kumupendeza [Mungu] vema.’ (Waebrania 11:6) Hiyo ni sababu kubwa kabisa yenye kutuchochea kuiga imani kubwa ya Enoko!

^ fu. 14 Wasomi fulani wa Biblia wanasema kama Yuda alitaja maneno yenye hayakuongozwa na roho ya Mungu ambayo yanapatikana katika kitabu chenye kuitwa Kitabu cha Enoko, lakini kitabu hicho kinajaa mambo ya kuwazia yenye hayajulikane kama yalitokea wapi. Kisha inasemekana kwa uongo kama ni Enoko ndiye aliandika kitabu hicho. Kitabu hicho kiko na maneno ya kweli ya unabii wenye Enoko alitoa. Inawezekana maneno hayo yalitoka katika maandishi ya zamani yenye yamekwisha kupotea; pengine maandishi hayo yalikuwa yenye kuandikwa ao yalikuwa mapokeo yenye yalipitishwa mudomo kwa mudomo. Inawezekana Yuda alitumia maandishi hayo ya zamani, ao pengine Yesu alimuelezea kuhusu Enoko, kwa sababu wakati alikuwa mbinguni, Yesu alijionea maisha ya Enoko duniani.

^ fu. 20 Vilevile Mungu alihakikisha kwamba hakuna mutu mwenye angetendea mwili wa Musa na mwili wa Yesu mambo kama hayo.—Kumbukumbu la Torati 34:5, 6; Luka 24:3-6; Yuda 9.