Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

TUIGE IMANI YAO | TIMOTHEO

‘Mutoto Wangu Mupendwa na Muaminifu Katika Bwana.’

‘Mutoto Wangu Mupendwa na Muaminifu Katika Bwana.’

TIMOTHEO alitembea kwenye barabara yenye kumupeleka mbali na kwao, macho yake yalikazia kwa hamu mambo yenye yalikuwa mbele. Wasafiri wenzake waliongoza safari wakati walipita katika maeneo yenye Timotheo alijua muzuri. Pole kwa pole waliacha nyuma yao muji wa Listra, wenye ulikuwa kwenye kilima kidogo katika bonde. Timotheo alicheka kidogo wakati aliwaza juu ya mama yake na tate (nkambo) yake mwanamuke, wenye walijivuna na kuficha machozi yao wakati walimuona anaenda. Alipaswa kugeuka na kuwapepea mara ya mwisho?

Mara kwa mara, mutume Paulo alikuwa anageuka na kumuangalia Timotheo na kucheka kidogo ili kumutia moyo. Alijua kama Timotheo alikuwa angali na haya yenye alipaswa kumaliza, lakini alifurahi kuona bidii ya kijana huyo. Timotheo alikuwa kijana sana, pengine alikuwa angali na miaka 20 hivi, na alimuheshimia Paulo na kumupenda sana. Sasa Timotheo alikuwa anafuata mwanaume huyo mwenye nguvu na muaminifu kwenye safari yenye ingemupeleka kilometre nyingi sana mbali na nyumbani. Wangefanya safari kwa miguu na kwa mashua (bateau) na wangepata hatari nyingi njiani. Timotheo hakujua kabisa kama angerudia nyumbani siku moja.

Ni nini kilifanya Timotheo afuatie maisha ya namna hiyo? Ni baraka gani zingefanya kujitoa hivyo kuwe kwa maana? Na namna gani tunaweza kuiga imani ya Timotheo?

‘TANGU UTOTO MUCHANGA’

Acha turudie miaka mbili ao tatu nyuma, na tuwazie kuwa Timotheo aliishi katika muji wa Listra; inawezekana ilikuwa hivyo. Ulikuwa muji mudogo, wenye maisha ya mashambani, uliokuwa katika bonde la mbali na lenye maji mengi. Inawezekana watu walikuwa wanajua luga ya Kigiriki, lakini walikuwa wanasema Kilikaonia, luga ya eneo lao. Siku moja kulitokea fujo katika muji huo wenye utulivu. Wamisionere wawili Wakristo, mutume Paulo na Barnaba mwenye alikuwa anasafiri naye, walifika Listra kutoka Ikoniamu, muji mukubwa wenye ulikuwa karibu. Wakati walikuwa wanahubiri mahali pa watu wengi, Paulo aliona mwanaume mwenye alikuwa kilema ambaye alionyesha imani ya kweli. Kwa hiyo, Paulo alifanya muujiza na kumuponyesha mwanaume huyo!—Matendo 14:5-10.

Pengine watu wengi wa Listra waliamini hadisi zao za kutunga zenye zilionyesha kama, wakati wa zamani, miungu ilijigeuza kuwa watu na kuja katika eneo lao. Kwa hiyo, watu waliwaza kimakosa kama Paulo alikuwa Herme na Barnaba alikuwa Zeu. Wakristo hao wawili wanyenyekevu walizuia watu kwa shida ili wasiwatolee zabihu.—Matendo 14:11-18.

Lakini watu fulani katika Listra hawakuona kuwa walikuwa wametembelewa na miungu ya kuwazia ya kipagani; waliona kuwa walitembelewa na watu wa kawaida na wenye kuleta habari ya muzuri. Kwa mufano, Eunike, mwanamuke Muyahudi mwenye alikuwa na bwana Mugiriki mwenye hakukuwa Mukristo, * pamoja na Loisi, mama yake, walimusikiliza Paulo na Barnaba kwa furaha na hamu kubwa. Paulo na Barnaba walikuja na habari hii yenye kila Muyahudi muaminifu alipenda kusikia: Masiya alikuwa amekuja na alikuwa ametimiza unabii mwingi wenye uliandikwa juu yake katika Maandiko!

Fikiria namna Timotheo aliguswa moyo wakati Paulo aliwatembelea. Timotheo alizoezwa ‘tangu utoto muchanga’ kupenda maandishi matakatifu ya Maandiko ya Kiebrania. (2Timotheo 3:15) Kama vile mama yake na tate yake, Timotheo aliona kuwa Paulo na Barnaba walisema kweli juu ya Masiya. Na fikiria mwanaume mwenye Paulo aliponyesha. Tangu wakati Timotheo alikuwa mutoto, inawezekana aliona mara nyingi mwanaume huyo kwenye barabara za Listra. Sasa Timotheo aliona mwanaume huyo anatembea kwa mara ya kwanza! Haishangaze kuona kama Eunike na Loisi walifikia kuwa Wakristo, na Timotheo pia. Leo, wazazi wa watoto na wazazi wa wazazi wao wanaweza kujifunza mengi kupitia mufano wa Loisi na Eunike. Munaweza kuwachochea vijana kwa njia ya muzuri?

‘KUPITIA ZIKI NYINGI’

Kwa kweli, watu wenye waligeuka kuwa Wakristo katika muji wa Listra walifurahi sana wakati walijua tumaini lenye wanafunzi wa Kristo walikuwa nalo. Lakini, walijifunza pia kama, kuwa mwanafunzi wa Yesu kunaleta mateso. Wapinzani Wayahudi wenye kushikilia imani yao kutoka Ikoniamu na Antiokia walikuja katika muji wa Listra, na walichochea wakaaji wa muji huo wapinge Paulo na Barnaba. Kisha muda kidogo, kikundi cha watu wenye hasira walimufuata Paulo na kumutupia majiwe. Paulo alipigwa sana, kisha akaanguka chini. Watu hao walimukokotea inje ya muji na kumuacha karibu kufa.—Matendo 14:19.

Hata hivyo, wanafunzi katika muji wa Listra walikuja na kuzunguka Paulo. Walifurahi sana wakati alijitikisa, akaamuka, na kisha bila woga akaenda tena katika muji wa Listra! Siku yenye ilifuata, Paulo na Barnaba walienda katika muji wa Derbe ili kuendelea na kazi ya kuhubiri. Kisha kufanya wanafunzi wapya huko pia, bila kuogopa hatari walirudia tena Listra. Kwa kusudi gani? Biblia inasema kama walirudia ili ‘kuzitia nguvu nafsi za wanafunzi, wakiwatia moyo kubakia katika imani.’ Wazia namna Timotheo alisikiliza, na kufungua macho kabisa, wakati Paulo na Barnaba walikuwa wanafundisha Wakristo hao kama tumaini lao la muzuri la wakati unaokuja linapita sana mateso ya wakati huo. Walisema hivi: ‘Lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia ziki [mateso] nyingi.’—Matendo 14:20-22.

Timotheo alisikiliza kwa moyo wote mafundisho ya mutume Paulo

Timotheo alikuwa ameona namna Paulo alikuwa anaishi kulingana na maneno hayo, kwa kupambana na mateso bila woga ili kutangazia wengine habari njema. Kwa hiyo, Timotheo alijua kama ikiwa angefuata mufano wa Paulo, watu wa Listra wangemupinga, na baba yake angemupinga pia. Lakini Timotheo hangeruhusu upinzani huo umuzuie kukamata uamuzi wa kumutumikia Mungu. Leo, vijana wengi wako kama Timotheo. Kwa hekima, wanatafuta marafiki wenye kuwa na imani ya nguvu, wenye watawatia moyo na kuwatia nguvu. Na hawaruhusu upinzani wenye wanapata uwazuie kumutumikia Mungu wa kweli!

“ALISHUHUDIWA VEMA NA AKINA NDUGU”

Kama vile imekwisha kuonyeshwa, inawezekana Paulo alitembelea tena Listra miaka mbili ao tatu baadaye. Fikiria furaha kubwa yenye ilitokea kwao Timotheo wakati Paulo alifika, mara hiyo alikuja pamoja na Sila. Kwa kweli, huo ulikuwa wakati wa furaha kwa Paulo pia. Paulo angeweza kujionea yeye mwenyewe namna mbegu za kweli zenye alipanda katika Listra zilikuwa zimekomaa. Katika muji huo kulikuwa Loisi na Eunike, mutoto wake mwanamuke, wenye sasa walikuwa wanawake Wakristo waaminifu, wenye “imani isiyo na unafiki” yenye Paulo alifurahia sana. (2 Timotheo 1:5) Na tuseme nini juu ya kijana Timotheo?

Paulo aliambiwa kama Timotheo alikuwa amefanya maendeleo ya muzuri ya kiroho tangu wakati aliwatembelea mara ya kwanza. Timotheo “alishuhudiwa vema [muzuri] na akina ndugu,” katika muji wa Listra na katika muji wa Ikoniamu, wenye ulikuwa kwenye kilometre karibu 32 kaskazini-mashariki. (Matendo 16:2) Namna gani Timotheo alipata sifa hiyo ya muzuri?

Kati ya “maandishi matakatifu” yenye Timotheo alifundishwa ‘tangu utoto muchanga’ na mama yake na tate yake mwanamuke, kulikuwa mashauri ya muzuri na yenye kufaa kwa ajili ya vijana. (2 Timotheo 3:15) Mufano mumoja ni huu: ‘Umukumbuke, sasa, Muumba wako Mukubwa katika siku za ujana wako.’ (Mhubiri 12:1) Timotheo alikamata maneno hayo kwa uzito kisha kuwa Mukristo. Aliona kama njia moja ya muzuri ya kumukumbuka Muumba wake Mukubwa ni kutangaza habari njema juu ya Kristo, Mwana wa Mungu. Pole kwa pole, Timotheo alijifunza kumaliza haya yake ya kizalikio na alijifunza kuambia wengine habari njema juu ya Yesu Kristo bila woga.

Wanaume wenye waliongoza katika makutaniko waliona maendeleo ya Timotheo. Kwa kweli, waliguswa moyo kuona namna kijana huyo alikuwa anajenga na kutia moyo kila mutu mwenye alikuwa karibu naye. Jambo la maana zaidi ni kwamba Yehova aliona maendeleo ya Timotheo. Kupitia roho yake, Mungu aliongoza unabii fulani utolewe juu yake, pengine kuhusu aina ya utumishi wenye angefanya siku moja katika makutaniko mengi. Wakati Paulo aliwatembelea, aliona kama Timotheo angeweza kusaidia sana kwa kusafiri pamoja naye katika safari zake za umisionere. Ndugu wa Listra walikubali jambo hilo. Waliweka mikono yao juu ya kijana huyo, alama yenye ilionyesha kama alichaguliwa kwa ajili ya pendeleo la pekee katika utumishi wa Yehova Mungu.—1 Timotheo 1:18; 4:14.

Tunaweza kuwazia kuwa Timotheo alishangaa kabisa na kunyenyekea kwa kutumainiwa sana na kupewa pendeleo hilo kubwa. Alikuwa tayari kuenda. * Namna gani baba yake mwenye hakukuwa Mukristo alitenda wakati mutoto wake alipata pendeleo hilo la kuwa mutumishi Mukristo mwenye kusafiri? Pengine alikuwa na mawazo mengi juu ya wakati unaokuja wa mutoto wake. Tuseme nini juu ya mama yake na tate yake mwanamuke? Walijivuna kwa ajili ya kijana huyo mwanaume na wakati uleule walijaribu kuficha mahangaiko yao juu ya usalama wake? Hilo lilikuwa jambo la kawaida.

Jambo la hakika ni kwamba Timotheo alienda. Asubui yenye kuzungumuziwa kwenye mwanzo wa habari hii, Timotheo alianza maisha ya kusafiri pamoja na mutume Paulo. Wakati aliacha Listra nyuma yake, kila kelele ya majiwe yenye alikanyaga na viatu vyake, mulio wa majani yenye alikanyaga, mambo hayo yote yalimaanisha hatua ingine yenye ilimupeleka kwenye hajue, mbali na kwao. Kisha kutembea muchana muzima, wanaume hao watatu walifika Ikoniamu. Sasa, Timotheo alianza kuona namna Paulo na Sila walikuwa wanatolea ndugu wa Ikoniamu maagizo ya mwisho-mwisho ya baraza lenye kuongoza lenye lilikuwa Yerusalemu, na namna walijenga imani ya waamini hao. (Matendo 16:4, 5) Lakini huo ulikuwa mwanzo tu.

Kisha kutembelea makutaniko katika Galatia, wamisionere hao waliacha barabara kubwa za Roma zenye kutiwa lami (kabulimbo), walitembea mamia ya kilometre katika maeneo makubwa yenye kuinuka ya Frigia, na wakaelekea kaskazini na kisha mangaribi. Kwa kufuata muongozo wa roho ya Mungu, walienda Troa, kisha wakapanda mashua mupaka Makedonia. (Matendo 16:6-12) Wakati huo, Paulo aliona kama Timotheo alikuwa wa lazima sana. Paulo alimuacha Timotheo pamoja na Sila katika muji wa Beroya. (Matendo 17:14) Hata alimutuma kijana huyo yeye peke Thesalonike. Timotheo alifuata mifano mizuri yenye alikuwa anaangalia kwa uangalifu, na alijenga Wakristo waaminifu huko.—1 Wathesalonike 3:1-3.

Kisha, Paulo aliandika juu ya Timotheo hivi: ‘Sina mutu mwengine yeyote aliye na muelekeo kama wake atakayejali [atakayehangaikia] kwa unyoofu mambo yenu.’ (Wafilipi 2:20) Sifa hiyo ya muzuri ya Timotheo haikutokea tu kwa muujiza. Lakini aliipata kupitia kazi ngumu, utumishi wa unyenyekevu, na kuvumilia kwa uaminifu katika magumu. Huo ni mufano muzuri sana kwa vijana leo! Musisahau hata siku moja kama ni ninyi wenyewe ndio munaweza kujifanyia sifa ya muzuri. Kama wewe ni kijana, uko na nafasi ya muzuri sana ya kujifanyia sifa ya muzuri kwa kutia Yehova Mungu pa nafasi ya kwanza katika maisha yako, na kwa kuwatendea wengine kwa upole na heshima.

‘FANYA KABISA YOTE UNAYOWEZA ILI UKUJE KWANGU’

Wakati alikuwa kijana, Timotheo alitoa maisha yake kwa ajili ya utumishi wa Kikristo

Kwa miaka karibu 14 hivi, Timotheo alipitisha wakati mwingi kwa kutumika pamoja na mutume Paulo, rafiki yake. Kama Paulo, yeye pia alipata hatari nyingi na furaha nyingi. (2 Wakorintho 11:24-27) Wakati fulani, Timotheo alifungwa hata kwa sababu ya imani yake. (Waebrania 13:23) Kama Paulo, yeye pia aliwahangaikia sana ndugu na dada wenzake Wakristo na aliwaonyesha upendo mwingi wenye kutoka moyoni. Ndio sababu Paulo alimuandikia hivi: ‘Ninayakumbuka machozi yako.’ (2 Timotheo 1:4) Kama Paulo, inaonekana Timotheo alijifunza ‘kulia pamoja na watu wanaolia,’ kwa kujitia pa nafasi yao ili kuwatia moyo na kuwatuliza muzuri zaidi. (Waroma 12:15) Ni muzuri kila mumoja wetu ajifunze kufanya hivyo!

Haishangaze kuona kama baada ya muda Timotheo alifikia kuwa mwangalizi Mukristo wa muzuri sana. Paulo alimupatia kazi ya kutembelea makutaniko ili kuyatia nguvu na kuyatia moyo na ili kuweka wanaume wenye kustahili kuwa wazee na watumishi wa huduma katika makutaniko.—1 Timotheo 5:22.

Paulo alimupenda Timotheo sana, alikuwa anamupatia kijana huyo mashauri mengi ya kumusaidia na yenye kuwa kama ya baba. Alimuomba Timotheo akomalishe zawadi zake za kiroho na aendelee kufanya maendeleo. (1 Timotheo 4:15, 16) Paulo alimutia moyo Timotheo asiruhusu ujana wake, na pengine haya yake ya kizalikio, vimuzuie kushikamana na yenye kuwa haki. (1 Timotheo 1:3; 4:6, 7, 11, 12) Na hata Paulo alimupatia mashauri juu ya namna ya kupambana na ugonjwa fulani wenye ulikuwa unamusumbua kwa ukawaida, pengine ugonjwa wa tumbo (estomac) wenye ulimuhangaisha mara kwa mara.—1 Timotheo 5:23.

Wakati ulifika ambapo Paulo alijua kama mwisho wa maisha yake ulikuwa karibu; pengine alikuwa karibu kuuawa. Alimutumia Timotheo barua ya mwisho yenye kuongozwa na roho ya Mungu. Ilikuwa pia na maneno haya yenye kugusa moyo sana: ‘Fanya kabisa yote unayoweza ili ukuje kwangu upesi.’ (2 Timotheo 4:9) Paulo alimupenda sana Timotheo; alimuita ‘mutoto wangu mupendwa na muaminifu katika Bwana.’ (1 Wakorintho 4:17) Haishangaze kama alipenda rafiki yake akuwe karibu naye wakati alikaribia kufa! Kila mumoja wetu anaweza kujiuliza, ‘Watu wananitafuta ili niwatie moyo wakati wanapata magumu?’

Timotheo aliweza kufika mbele ya wakati ili kumuona Paulo? Hatujue. Lakini tunajua kama sikuzote alifanya yake yote ili kumutia Paulo moyo na kumutuliza, na alifanya hivyo kwa wengine wengi. Aliishi kupatana na maana ya jina Timotheo, lenye kumaanisha, “Mutu Mwenye Kuheshimia Mungu.” Na alituachia sisi wote, vijana na wazee, mufano muzuri sana wa imani wa kuiga.

^ fu. 9 Soma habari “Ulijua?” katika gazeti hili.

^ fu. 20 Timotheo alikubali hata kutahiriwa wakati Paulo alimuomba afanye hivyo. Kama alikubali, haiko kwa sababu jambo hilo liliombwa kwa Wakristo, lakini ni kwa sababu Paulo hakutaka Wayahudi wenye wangeenda kuhubiria wawapinge kwa sababu ya kuona kijana huyo mwenye baba yake hakukuwa Muyahudi.—Matendo 16:3.