Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Alikuwa wa Jamaa ya Kayafa

Alikuwa wa Jamaa ya Kayafa

Mara nyingi, watu wanaochimba vitu vya zamani wanavumbua vitu vilivyo na maandishi yanayoonyesha mambo fulani ao watu fulani wanaozungumuziwa katika Biblia. Kwa mufano, katika mwaka wa 2011, watu wenye elimu ya mambo hayo huko Israël walitangaza habari kuhusu uvumbuzi fulani kama huo. Jambo hilo ni sanduku la kuzikia lenye kupakwa chokaa lililotumiwa miaka 2 000 hivi iliyopita, ambamo walikuta mifupa ya mutu aliyekufa.

Sanduku hilo lilikuwa na maandishi haya: “Miriamu binti ya Yeshua mwana wa Kayafa, kuhani wa Maazia wa Beth-Imri.” Yule kuhani mukubwa Muyahudi aliyehusika na kusambishwa kwa Yesu na kuuawa kwake, alikuwa Kayafa. (Yoh. 11:48-50) Mwanahistoria Flavius Josèphe anamuita “Yosefu, aliyeitwa Kayafa.” Inaonekana kwamba sanduku hilo lilikuwa la mutu wa jamaa yake. Maandishi yaliyokuwa juu ya sanduku lililovumbuliwa mbele, lililozaniwa kuwa la kuhani mukubwa, yanamuita Yehosefu bar Kayafa, ao Yosefu mwana wa Kayafa. * Kwa hiyo, inawezekana Miriamu alikuwa na uhusiano na Kayafa kwa njia fulani.

Kulingana na habari iliyotolewa na Mamlaka ya Mambo ya Zamani ya Israël, sanduku la mifupa la Miriamu lilichukuliwa mikononi mwa wezi waliokuwa wakichimba makaburi ya zamani. Uchunguzi wa sanduku hilo na maandishi yake unaonyesha kwamba habari hiyo ni ya kweli.

Maandishi kwenye sanduku hilo yanatufunulia habari fulani mupya. Maandishi hayo yanataja kikundi cha makuhani wa jamaa ya “Maazia,” kikundi cha mwisho kati ya vikundi 24 vya makuhani waliokuwa wakigomboana kwenye hekalu la Yerusalemu. (1 Nya. 24:18) Maandishi hayo yanaonyesha kwamba “jamaa ya Kayafa ilikuwa katika kikundi cha Maazia.”

Maandishi kwenye sanduku hilo yanataja pia jina Beth-Imri. Kuna mawazo mawili kuhusu jina hilo. Wazo la kwanza kulingana na Mamlaka ya Mambo ya Zamani ya Israël ni kwamba “Beth-Imri ni jina la jamaa ya kikuhani ya watoto wa Imeri (Ezra 2:36-37; Neh. 7:39-42) ambao wajukuu wao walikuwa makuhani wa kikundi cha Maazia. Na wazo la pili ni kwamba Beth-Imri ni jina la mahali ambapo Miriamu ao jamaa yao yote iliishi.” Hata mafasirio yawe gani, sanduku la mifupa ya Miriamu linaonyesha wazi kwamba watu wanaozungumuziwa katika Biblia ni watu walioishi kabisa na waliokuwa na jamaa zao.

^ Ili kupata habari kuhusu sanduku la mifupa ya Kayafa, soma habari yenye kichwa ‘Kuhani Mukubwa aliyemuhukumu Yesu’ katika Munara wa Mulinzi wa 15/01/2006, ukurasa wa 10-13.