Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mambo Ambayo Unapaswa Kujua Juu ya Ugonjwa wa Kifafa

Mambo Ambayo Unapaswa Kujua Juu ya Ugonjwa wa Kifafa

MUTU unayefahamiana naye anaanguka chini na kuzimia. Mwili wake unakauka, na kisha anaanza kutikisa-tikisa kichwa, mikono na miguu yake. Ikiwa unajua kwamba mutu huyo ana ugonjwa wa kifafa, kwanza unaweza kumusaidia mbele apate musaada wa muganga. Tuzungumuzie basi mambo fulani ya hakika juu ya ugonjwa huo ambao mara nyingi watu hawaelewe vizuri.

Ugonjwa wa kifafa ni nini? Ugonjwa wa kifafa ni tatizo la ubongo ambalo linatokeza mashambulizi ya muda mufupi yanayoitwa kushikwa na kifafa. Mara nyingi kushikwa na kifafa hakupitishe dakika tano. Hali inayoelezwa mwanzoni mwa habari hii ni mufano wa kile kinachoitwa kifafa kikubwa.

Ni nini kinatokeza kushikwa na kifafa? Wachunguzi wanaamini kwamba kushikwa na kifafa kunatokea wakati kunakuwa ongezeko lisilo la kawaida la utendaji katika chembe za ubongo. Mupaka sasa wachunguzi hawaelewe sababu gani kunakuwa ongezeko hilo la utendaji katika chembe za ubongo.

Ikiwa ninaona mutu fulani anashikwa na kifafa kikubwa, ninaweza kufanya nini? Kitabu kimoja kinasema hivi: “Watu wanaotazama wanapaswa kumuacha mutu huyo amalize kujitikisa​-tikisa na kuepuka kumubana​-bana. Hata hivyo, wanapaswa kuchunguza ili kuhakikisha kwamba mutu huyo hayuko katika hatari ya kujiumiza kimwili na kwamba anaweza kupumua.” (The Encyclopedia of the Brain and Brain Disorders) Kwa upande mwengine, kitabu hicho kinasema hivi: “Motokari ya kubeba wagonjwa inapaswa kuitwa ikiwa kushikwa na kifafa kunafanya zaidi ya dakika tano, ao ikiwa anashikwa tena na kifafa mara moja baada ya kushikwa na kifafa kwa mara ya kwanza, ao ikiwa mutu harudiliwe na ufahamu dakika chache kisha hali ya kushikwa na kifafa kumalizika.”

Ninaweza kumusaidia mugonjwa wa kifafa namna gani wakati anashikwa na kifafa? Weka kitu kilicho laini kati ya kichwa chake na udongo, na uondoe vitu ambavyo vinaweza kumuumiza karibu na kichwa chake. Wakati anaacha kujitikisa​-tikisa, umugeuzie upande mwengine kama inavyoonyeshwa kwenye picha.

Ninaweza kufanya nini kisha mugonjwa kuamuka? Kwanza, umuhakikishie kwamba mambo yote ni sawa. Kisha, umusaidie kusimama na kumuongoza mahali ambapo anaweza kupumuzika. Watu wengi wanavurugika na wanasikia usingizi kisha kushikwa na kifafa; wengine wanarudilia hali yao ya kawaida haraka na wanaweza kuendelea kufanya kazi ambayo walikuwa wanafanya mbele ya kushikwa na kifafa.

Je, watu wote wanaoshikwa na kifafa wanaanguka na kujitikisa​-tikisa? Hapana. Wagonjwa fulani wanakuwa katika hali ya kupoteza ufahamu bila hata kuanguka chini. Hali hiyo inaitwa kifafa kidogo (ao kifafa ambacho hakimuangushe mutu), ambacho kwa kawaida ni kifupi na hakina matokeo mabaya yenye kudumu kwa muda murefu. Watu fulani walio na ugonjwa huo wanashikwa na kifafa kidogo mara nyingi kwa siku, ambacho kinaendelea kwa dakika nyingi. Katika hali hiyo, mugonjwa anaweza kutanga​-tanga katika chumba, kukokota nguo zake, ao kufanya mambo mengine yasiyo ya kawaida. Kisha kushikwa na kifafa, anaweza kusikia kizungu​-zungu.

Watu walio na ugonjwa wa kifafa wanapambana na magumu gani? Inaeleweka kwamba watu wengi walio na ugonjwa wa kifafa wanaishi na woga kwa sababu hawajue ni wakati gani na wapi kifafa kitawashikia tena. Ili kuepuka kupatwa na haya, wanaweza kuwa na mwelekeo wa kuepuka kuwa mahali pa watu wengi.

Ninaweza kumutegemeza namna gani mutu fulani aliye na ugonjwa wa kifafa? Umutie moyo asifiche namna anavyojisikia moyoni. Umusikilize vizuri anapozungumuza na wewe. Umuulize ikiwa angependa umufanyie nini anaposhikwa na kifafa. Kwa sababu watu wengi walio na ugonjwa wa kifafa hawatembeze motokari, labda unaweza kumubeba katika motokari yako ao kumufanyia kazi fulani.

Je, hali ya kushikwa na kifafa inaweza kupunguzwa na hata kuzuiwa? Mambo fulani yanaongeza uwezekano wa kushikwa na kifafa, kama vile mahangaiko ya maisha na kukosa usingizi. Kwa sababu hiyo, watu wenye elimu wanatia moyo watu walio na ugonjwa wa kifafa kulala vya kutosha na kufanya mazoezi ya mwili kwa ukawaida ili kupunguza mahangaiko ya maisha. Katika hali fulani, dawa pia zimesaidia kuzuia hali ya kushikwa na kifafa.