Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUU

Kuhamia Nchi Nyingine—Matarajio na Mambo Halisi

Kuhamia Nchi Nyingine—Matarajio na Mambo Halisi

Kutafuta Maisha Bora

GEORGE alikuwa ametamauka. Hangeweza kupata chakula cha kutosha kwa ajili ya familia yake. Wakati huohuo, majirani walikuwa wanaugua, na wengine walionekana kuwa wenye njaa. Hata hivyo, kulikuwa na nchi tajiri kilomita chache upande wa kusini. George alijiambia hivi, ‘Nitahamia nchi hiyo, nitafute kazi, kisha familia yangu itajiunga nami.’

Patricia pia alikuwa amefikiria kuanza maisha mapya ng’ambo. Hakuwa na kazi na kulikuwa na nafasi chache sana za kuboresha maisha yake. Yeye na rafiki yake wa kiume waliamua kusafiri kutoka Nigeria hadi Algeria, wakielekea Hispania, bila kujua kwamba safari ya kuvuka Jangwa la Sahara ingekuwa ngumu sana. Alisema hivi, “Nilikuwa mja-mzito na nilikuwa nimeazimia kumpa mtoto wangu maisha bora.”

Rachel alitaka kuboresha hali yake ya kiuchumi kwa kuhamia Ulaya. Alikuwa amepoteza kazi yake huko Filipino, na watu wake wa ukoo walimhakikishia kwamba kulikuwa na nafasi nyingi za kupata kazi za nyumbani ng’ambo. Alikopa pesa za nauli ya ndege na kumuaga mume na binti yake na kuwaahidi hivi, “Tutaonana tena hivi karibuni.”

Inakadiriwa kwamba kama George, Patricia, na Rachel, zaidi ya watu milioni 200 wamehamia ng’ambo katika miaka ya karibuni. Ingawa baadhi yao wamefanya hivyo ili kukimbia vita, misiba ya asili, au kunyanyaswa, wengi wamehamia huko kwa sababu za kiuchumi. Wahamiaji wamekabili matatizo gani katika nchi walizohamia? Je, ni wote wanaofaulu kupata maisha bora waliyokuwa wakitafuta? Watoto huathiriwaje wazazi wanapowaacha ili kwenda kuboresha hali yao ya kiuchumi? Chunguza majibu yafuatayo ya maswali hayo.

Safari ya Kufika Huko na Kuanza Maisha

Tatizo la kwanza ambalo mtu hukabili anapohamia ng’ambo ni safari yenyewe. George, aliyetajwa katika makala iliyotangulia, alisafiri mamia ya kilomita akiwa na chakula kidogo tu. Anasema hivi, “Safari hiyo ilikuwa ngumu sana.” Wahamiaji wengi hata hawafiki wanakoenda.

Patricia alikusudia kwenda Hispania. Alisafiri ndani ya lori lililokuwa wazi nyuma kupitia Jangwa la Sahara. “Safari ya kutoka Nigeria hadi Algeria ilichukua juma moja, na watu 25 walisongamana katika lori hilo. Tulipokuwa njiani, tuliona maiti nyingi na pia watu waliokuwa wakiranda-randa jangwani wakingojea kufa. Inaonekana kwamba madereva fulani wa lori wasiokuwa na huruma huwaacha abiria wao njiani.”

Tofauti na George na Patricia, Rachel alisafiri kwa ndege hadi Ulaya, ambapo angefanya kazi za nyumbani. Lakini hakuwa amewazia jinsi ambavyo angemkosa sana binti yake mwenye umri wa miaka miwili. Anasema, “Kila mara nilipomwona mama akimtunza mtoto wake mchanga, nilijawa na huzuni.”

George alijitahidi sana kuzoea maisha katika nchi aliyohamia. Ilimchukua miezi kadhaa kabla ya kupata pesa za kutuma nyumbani. Anakiri hivi, “Nililia sana usiku kwa sababu ya upweke na kukata tamaa.”

Baada ya kukaa miezi kadhaa nchini Algeria, Patricia alifika mpakani mwa Morocco na Algeria. Anasema: “Nikiwa huko nilijifungua mtoto wa kike. Ilibidi nijifiche ili nisikamatwe na watu wanaowateka nyara wanawake wahamiaji na kuwalazimisha kuwa makahaba. Mwishowe, nilipata pesa za kutosha kufunga safari hatari ya kuvuka bahari kwa mashua hadi Hispania. Mashua hiyo haikuwa katika hali nzuri na haikukusudiwa kubeba abiria wengi. Ilibidi tuzoe maji kutoka kwenye mashua hiyo kwa kutumia viatu vyetu! Tulipofika kwenye pwani ya Hispania, sikuwa na nguvu za kutembea hadi ufuoni.”

Bila shaka, watu wanaopanga kuhamia nchi nyingine wanapaswa kufikiria mengi zaidi ya hatari zinazohusianishwa na safari ya kwenda huko. Wanapaswa kufikiria pia matatizo watakayopata kwa sababu ya lugha na tamaduni za nchi mpya, na pia gharama na matatizo ya kisheria ya kujaribu kuwa raia au wakaaji wa kudumu wa nchi hiyo. Wale ambao hawapati vibali halali vya kuishi katika nchi hizo mara nyingi inakuwa vigumu kwao kupata kazi nzuri, nyumba nzuri, elimu, au hata huduma za afya. Pia huenda ikawa vigumu kwao kupata leseni ya kuendesha gari au kufungua akaunti ya benki. Mara nyingi wahamiaji wasio na vibali halali hutumiwa vibaya na kulipwa mishahara midogo sana.

Jambo lingine ambalo mtu anapaswa kufikiria ni pesa. Je, tunapaswa kuweka tumaini letu katika pesa? Biblia inatoa shauri hili lenye hekima: “Ikiwa unayo hekima ya kutosha, usijitaabishe kutafuta utajiri. Kufumba na kufumbua utajiri hutoweka, huwa kama umepata mabawa ghafla, ukaruka na kutowekea angani kama tai.” (Methali 23:​4, 5, Biblia Habari Njema) Pia, kumbuka kwamba uhitaji wetu mkubwa ni mambo ambayo hayawezi kununuliwa kwa pesa, yaani, upendo, usalama wa kihisia, na umoja wa familia. Inasikitisha kama nini wazazi wanapoacha tamaa ya pesa iwe ndilo jambo muhimu kuliko upendo wao kwa wenzi wao au “upendo wa asili” kwa watoto wao!​—⁠2 Timotheo 3:1-3.

Pia, wanadamu wana uhitaji wa kiroho. (Mathayo 5:3) Hivyo, wazazi wanaochukua mambo kwa uzito hufanya kila wawezalo ili kutimiza daraka walilopewa na Mungu la kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu, kusudi lake, na viwango vyake.​—Waefeso 6:4.

Familia Yenye Umoja Ni Muhimu Zaidi Kuliko Pesa

Huenda masimulizi ya wahamiaji yakatofautiana, lakini mengi huwa na matokeo yaleyale, kama masimulizi ya George, Rachel, na Patricia, waliotajwa katika makala zilizotangulia za mfululizo huu yanavyoonyesha. Familia huumia mzazi anapoondoka au mwenzi wa ndoa anapomwacha mwenzake, na huenda ikachukua miaka mingi kwa familia kuungana tena. Katika kisa cha George, ilichukua zaidi ya miaka minne kwa familia yake kujiunga naye.

Mwishowe Rachel alirudi Filipino na kumchukua binti yake baada ya kutengana naye kwa karibu miaka mitano. Patricia aliwasili Hispania akiwa na binti yake mchanga. Anasema hivi, “Yeye tu ndiye mtu wa familia niliye naye, kwa hiyo ninajitahidi kumtunza vizuri.”

Wahamiaji wengi hujitahidi kuishi katika nchi waliyohamia licha ya upweke, matatizo ya kiuchumi, na kutengana kwa muda mrefu na familia zao. Kwa kuwa wametumia wakati, nguvu, na pesa nyingi kuhamia huko, ni wachache sana huwa na ujasiri wa kurudi nyumbani na kukabili fedheha na aibu ikiwa mambo yatawaendea mrama ng’ambo.

Allan, kutoka Filipino alipata ujasiri wa kurudi nyumbani. Alipata kazi nzuri nchini Hispania, lakini baada ya miezi 18, alirudi nyumbani. Anasema hivi: “Niliwakosa sana mke na binti yangu mchanga. Niliamua sitafanya tena kazi ng’ambo isipokuwa nihame pamoja na familia yangu. Na tulifanya hivyo hatimaye. Familia ni muhimu zaidi kuliko pesa.”

Patricia aligundua jambo lingine lililo muhimu zaidi kuliko pesa. Alipofika Hispania, alikuwa na nakala ya “Agano Jipya,” au Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Alisema: “Niliona kitabu hicho kama hirizi ya kunilinda. Kisha nikakutana na mwanamke mmoja aliyekuwa Shahidi wa Yehova. Zamani, sikupendezwa kuzungumza na Mashahidi. Kwa hiyo nilimwuliza Shahidi huyo maswali mengi ili nimwonyeshe kwamba yale anayoamini si sahihi. Lakini, tofauti na nilivyotarajia, aliitetea imani yake na kujibu maswali yangu kwa kutumia Biblia.”

Patricia alijifunza kwamba kuwa na furaha ya kudumu na tumaini hakika la wakati ujao hakutegemei mahali mtu anapoishi au pesa bali kunategemea kumjua Mungu na kusudi lake kwa ajili yetu. (Yohana 17:3) Baadhi ya mambo ambayo Patricia alijifunza ni kwamba Mungu wa kweli ana jina​—Yehova. (Zaburi 83:18) Pia alisoma katika Biblia kwamba hivi karibuni, kupitia serikali yake ya Ufalme iliyo chini ya Yesu Kristo, Mungu ataondoa umaskini wote. (Danieli 7:13, 14) Zaburi 72:12, 14 inasema: “[Yesu] atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.”

Mbona usitenge wakati wa kuichunguza Biblia? Kitabu hicho chenye hekima kutoka kwa Mungu kinaweza kukusaidia kujua mambo yaliyo muhimu zaidi maishani mwako, kufanya maamuzi yenye hekima, na kuvumilia majaribu yoyote ya sasa kwa shangwe na tumaini.​—Methali 2:​6-9, 20, 21.