Ona video zinazopatikana

Yesu Alifanana Namna Gani?

Yesu Alifanana Namna Gani?

Jibu la Biblia

 Hakuna mutu mwenye anajua muzuri namna Yesu alifanana, kwa sababu Biblia haizungumuzie sura na umbo lake. Hilo linaonyesha kwamba sura na umbo la Yesu hayako mambo ya maana. Lakini, Biblia inatutolea mawazo fulani kuhusu namna Yesu alifanana kwa ujumla.

  •   Sura na umbo: Yesu alikuwa Muyahudi na bila shaka aliriti umbo la kiyahudi kutoka kwa mama yake. (Waebrania 7:14) Inawezekana sura na umbo lake havikuwa tofauti kabisa na watu wengine. Wakati fulani alifikia kusafiri kwa siri kutoka Galilaya mupaka Yerusalemu bila hata watu kumutambua. (Yohana 7:​10, 11) Na inaonekana kwamba hata kati ya mitume wake, hakuwa na umbo lenye kuwa tofauti sana nao. Kumbuka kwamba, Yuda Iskariote alipaswa kumutambulisha kwenye kikundi cha watu wenye walikamata Yesu.​—Mathayo 26:47-​49.

  •   Urefu wa nywele: Inawezekana Yesu hakuwa na nywele ndefu, kwa sababu Biblia inasema kwamba “nywele ndefu, ni aibu [kwa mwanaume].”​—1 Wakorintho 11:14.

  •   Ndevu: Yesu alikuwa na ndevu. Alifuata sheria ya Wayahudi yenye ilikataza wanaume ‘kuharibu ncha ya ndevu zao.’ (Mambo ya Walawi 19:27; Wagalatia 4:4) Pia, Biblia inaeleza kuhusu ndevu za Yesu katika unabii wenye kuzungumuzia mateso yake.​— Isaya 50:6.

  •   Mwili: Maelezo yote yanaonyesha kwamba Yesu alikuwa na nguvu. Wakati wa utumishi wake, alisafiri kilometre nyingi. (Mathayo 9:​35) Mara mbili alisafisha hekalu la Wayahudi akipindua meza za wabadilisha-feza, na mara moja alifukuza inje wanyama kwa kutumia fimbo. (Luka 19:45, 46; Yohana 2:​14, 15) Kitabu Cyclopedia cha McClintock na Strong kinasema hivi: “Maelezo yote ya injili yanaonyesha [Yesu] akiwa na afya nzuri na nguvu nyingi za kimwili.”​—Buku la IV, ukurasa wa 884.

  •   Ishara za uso: Yesu alikuwa mwenye shauku na mwenye huruma, na bila shaka hilo lilionekana kupitia ishara za uso wake. (Mathayo 11:28, 29) Watu wa namna zote walimutafuta ili kupata kitulizo na musaada. (Luka 5:​12, 13; 7:3​7, 38) Hata watoto walijisikia muzuri kuwa pamoja naye.​—Mathayo 19:13-​15; Marko 9:​35-​37.

Mawazo ya uongo kuhusu sura na umbo la Yesu

 Wazo la uongo: Watu fulani wanasema kwamba Yesu alikuwa wa kizazi cha Waafrika kwa sababu kitabu cha Ufunuo kinafananisha nywele zake na sufu (ao, manyoya ya kondoo) na miguu yake na “shaba inapowaka.”​—Ufunuo 1:​14, 15.

 Ukweli wa mambo: Kitabu cha Ufunuo kinatolewa “kwa njia ya ishara.” (Ufunuo 1:1) Maelezo kuhusu nywele na miguu ya Yesu ni maneno ya mufano yenye kuonyesha sifa zake kisha ufufuo wake, haiko maelezo kuhusu sura na umbo lake wakati alikuwa katika dunia. Wakati inasema kwamba “kichwa chake na nywele zake zilikuwa nyeupe kama sufu nyeupe, kama theluji,” Ufunuo 1:​14 inatumia rangi kuwa ulinganifu, hapana umbo la nywele. Hilo linaonyesha hekima yake yenye kutokana na miaka yake. (Ufunuo 3:​14) Andiko hili halilinganishe umbo la nywele za Yesu na sufu na halilinganishe pia umbo la nywele zake na teluji.

 Miguu ya Yesu ilionekana “kama shaba safi inapowaka katika tanuru.” (Ufunuo 1:​15) Pia, sura yake ilikuwa “kama jua linapoangaza katika nguvu zake.” (Ufunuo 1:​16) Kwa kuwa hakuna watu wenye kuwa na rangi ya ngozi yenye kupatana na maelezo hayo, maono hayo yanapaswa kuwa ya mufano, na yanaonyesha Yesu mwenye kufufuliwa kama mutu “anayekaa katika nuru isiyoweza kufikiwa.”​—1 Timotheo 6:​16.

 Wazo la uongo: Yesu alikuwa muzaifu.

 Ukweli wa mambo: Kila mara Yesu alitenda kama mwanaume. Kwa mufano, alijitambulisha bila kuogopa kwa kikundi cha watu wenye walikuja kumukamata. (Yohana 18:4​-8) Yesu alipaswa kuwa na nguvu kwa sababu alifanya kazi ya useremala kwa kutumia vyombo vyenye havitumie umeme.​—Marko 6:3.

 Sasa, sababu gani Yesu alikuwa na lazima ya musaada ili kubeba muti wake wa mateso? Na sababu gani alikufa mbele ya watu wengine wenye walihukumiwa pamoja naye? (Luka 23:26; Yohana 19:31-​33) Mbele ya kifo chake, mwili wake ulikuwa umefanywa zaifu sana. Hakulala usiku muzima, kwa upande fulani kwa sababu ya maumivu makali ya hisia. (Mathayo 26:67, 68; Yohana 19:​1-3) Usiku Wayahudi walimutendea mubaya, na asubui yenye kufuata Waroma walimutesa sana. (Mathayo 26:67, 68; Yohana 19:​1-3) Bila shaka mambo hayo yalifanya akufe haraka.

 Wazo la uongo: Sikuzote Yesu alikuwa mwenye huzuni.

 Ukweli wa mambo: Yesu alionyesha kwa ukamilifu sifa za Baba yake wa mbinguni, Yehova, ambaye Biblia inamutaja kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:​11; Yohana 14:9) Kwa kweli, Yesu alifundisha wengine namna ya kuwa na furaha. (Mathayo 5:​3-9; Luka 11:28) Mambo hayo yanaonyesha kwamba kila mara ishara za uso wake zilionyesha furaha.